TUMUSIFU BWANA

prop

Tuesday 5 June 2018

Kocha simba akataa kupangiwa

Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa kudownload APP YETU BOFYA HAPA, Au ingia playstore tafuta KALAMBO NEWS kisha bofya install.

SIKU za kocha Pierre Lechantre kuendelea kuifundisha Simba zinahesabika baada ya viongozi wa timu hiyo pamoja na wachezaji kueleza kuchoshwa na baadhi ya tabia za Mfaransa huyo, huku kubwa likiwa ni kutokubali kuingiliwa katika suala zima la upangaji kikosi.


kocha Pierre Lechantre.

Lechantre alichukua majukumu ya kuinoa timu hiyo raundi ya pili ya msimu uliomalizika akisaidiwa na Masoud Djuma ambapo kwa pamoja wameisaidia Simba kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu wa 2017/18 huku timu hiyo ikimaliza ligi kwa kupoteza mechi moja tu kati 30.


Taarifa kutoka ndani ya klabu hiyo kupitia kwa baadhi ya viongozi wa timu hiyo waliopo mjini hapa, zinaeleza kuwa tabia ya kocha huyo ya kubagua wachezaji imewakera na pia hashauriki kila anapopewa ushauri juu ya jambo fulani.

Mmoja wa viongozi hao aliliambia Nipashe jana kuwa, tabia hiyo imeifanya Simba pamoja na kupata ushindi au kutopoteza michezo bado timu haichezi ikiwa na uhakika wa ushindi.

"Timu inashinda, lakini kuanzia dakika ya kwanza ya mchezo mpaka mpira unamalizika, tunakuwa na presha kutokana na aina ya mchezo tunaocheza na pia wachezaji anaowatumia," alisema kiongozi huyo ambaye hakutaka jina lake kutajwa gazetini.

Alisema wapo wachezaji ambao hawana uwezo au uwezo wao upo chini, lakini kocha Lechantre ameendelea kuwang'ang'ania na kuwaacha baadhi ya wachezaji wanaojituma uwanjani na pia hataki ushauri wa watu wengine kwenye benchi la ufundi.

"Tazama mchezo wa jana (juzi, dhidi ya Kariobang Sharks katika michuano ya SportPesa Super Cup, timu inacheza kwa pasi tu lakini golini hawafiki, ukiangalia kwenye benchi kuna wachezaji wenye uwezo mkubwa, alimuingiza Marcel (Boniventura) na alionyesha kiwango kikubwa na timu ikabadilika baada ya kuingia yeye, lakini cha kushangaza baada ya dakika ya 20 tu akamtoa...,kocha ana mapenzi na baadhi ya wachezaji na amekuwa akiweka matabaka," alisema.

Alisema viongozi wanapenda kuiona timu inashinda na inafanya vizuri kama ilivyo kwa mashabiki na wanapofanya maamuzi ya kumfukuza kocha wanakuwa na sababu.

"Vyombo vya habari mnapaswa kutuelewa, tukibadilisha makocha huwa mnatusema sisi viongozi na mnatulalamikia sana, lakini mambo kama haya hatuwezi kuyavumilia, anatupa presha," alisema kiongozi huyo.

Hata hivyo, Lechantre akizungumza na gazeti hili mjini hapa, alifafanua kuwa aliamua kumtoa Marcel kwenye mchezo wa juzi kutokana na mchezaji huyo kutofuata maelekezo yake baada ya kumuingiza uwanjani.

Aidha, alisema wachezaji ndio askari wake kwenye vita, hivyo hawezi kumbagua yeyote kwa kuwa wote anawahitaji.

"Kila mchezaji anapata nafasi kutokana na uwezo wake, kujituma na namna anavyofuata maelekezo," alisema Lechantre.

Mkataba wa Lechantre na Simba unamalizika Juni 18, mwaka huu.

1 comment: